test

Thursday, July 7, 2016

Gesi Ya Kupikia Kuagizwa kwa Pamoja Kuanza Septemba

Serikali itaanza kutumia mfumo wa uagizaji wa pamoja wa nishati ya gesi ya kupikia (LPG), kama inavyofanyika kwa mafuta ya ndege, petroli, dizeli na mafuta taa ifikapo Septemba mwaka huu. 
Akizungumza wakati wa semina ya wadau wa sekta ya mafuta kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa, Mkurugenzi wa Petroli wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), Godwin Samuel alisema mpango huo utasaidia kupunguza gharama na bei ya gesi hiyo inayoanza kutumika kwa kasi majumbani. 
Samuel alisema mpango huo pia utaongeza udhibiti wa mapato ya Serikali katika sekta hiyo inayoshika kasi nchini. 
Kuhusu uagizaji wa mafuta ya ndege, petroli, dizeli na mafuta ya taa, Mkurugenzi huyo alisema mchakato unaendelea kuboresha mfumo wa sasa kwa kukusanya maoni na mapendekezo ya wadau yatakayotumika kubadilisha taratibu zilizopo ifikapo Novemba, mwaka huu mikataba ya sasa itakapomalizika.
“Tunakusudia kuongeza ushindani wenye tija katika uagizaji wa pamoja wa mafuta ya ndege, petroli, dizeli na mafuta taa kwa kuongeza idadi ya kampuni kulinganisha na kandarasi zilizopo zinazofikia kikomo ifikapo Novemba mwaka huu,” alisema Samuel. 
Kuhusu elimu kwa wadau, Mkurugenzi huyo alisema Ewura inalenga kuwawezesha kujua na kuzingatia mabadiliko yanayotokea katika sekta na biashara ya mafuta ili kuwezesha kila upande kutimiza wajibu kulingana na sheria, kanuni na taratibu. 
“Changamoto zinazoikabili sekta na biashara ya mafuta hayawezi kutatuliwa na Ewura pekee bali ni kwa ushirikiano wa wadau wote,” alisema.
TANGAZA HAPA KWA BEI NAFUU