test

Wednesday, June 15, 2016

Simu feki kizaazaa: kufungiwa leo saa 6 Usiku>>soma hapa zaidi!


WAKATI kesho Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ikitarajiwa kutimiza azma yake ya kuzima simu ‘feki’ za mkononi, upo mtikisiko na kizaazaa miongoni mwa watumiaji wa vifaa hivyo vya mawasiliano, wakisaka mbadala na wengine wakisubiri
kuona kama ‘yatatimia’.
Ingawa uzimaji wa simu bandia na kuanza kutumika kwa teknolojia mpya ya simu za mkononi kwa Mfumo wa Rajisi, unatarajiwa kuwa muarobaini wa wizi kwa simu za mkononi na kiama kwa watukanaji, watumaji picha chafu, baadhi ya wanajamii wanaipokea hatua hiyo kwa mtazamo hasi, wakiangalia hasara watakayopata baada ya simu zao kufungiwa.
Kizaazaa kimekumba siyo tu watumiaji wa simu, hususan wale ambao wameshabaini kuwa simu zao ni bandia, bali pia wenye maduka ya simu ambao baadhi inadaiwa kusafirisha simu hizo kwenda kuziuza nchi jirani.
Wakati hayo yakijiri miongoni mwa watumiaji wa simu za mkononi, kwa upande wao, kampuni za simu za mkononi zimetumia fursa hiyo kufanya biashara ya simu za mkononi kwa bei nafuu, itakayowezesha wenye kipato cha chini kumudu bei yake.
Watamani siku ifike
Baadhi ya wafanyabiashara wa simu jijini Dar es Salaam waliozungumza na gazeti hili, walieleza matamanio yao ya kuzimwa simu bandia ili biashara yao iendelee, kwa kile walichosema imedorora tangu TCRA ilipotangaza uamuzi wake.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, walisema kumekuwa na hofu miongoni mwa wateja ambao wengi wanachelea kununua simu kutokana na hofu ya kuuziwa zilizo bandia.
“Tangu mwanzoni mwa mwaka huu, biashara ya simu imeyumba kwa kiasi kikubwa kutokana na tangazo la TCRA,” alisema Mohammed Bakari ambaye hata hivyo alisema binafsi anauza simu halali, ambazo pia zimekosa soko kama ilivyo kawaida kutokana na kuhofia za bandia.
Mfanyabiashara mwingine, Erick Ngamwe alisema, uamuzi wa serikali wa kuzima simu hizo ni jambo zuri. Alishauri isitoe muda wa ziada ambao kwa mujibu wake, utaendelea kuyumbisha biashara yao.
Hata hivyo, mfanyabiashara mwingine wa Kariakoo, Nassor Said alisema, wapo baadhi yao ambao wataumia kwa kuwa walikuwa na mzigo mkubwa wa bidhaa hiyo.
“Hili tunaliona jambo zuri lakini kuna watu wanaumia, watu walikopa fedha kuagiza mzigo wa simu leo hii hajamaliza hata kerejesha pesa yote, simu zinazimwa na anakuwa anapata hasara, kwahiyo si jambo la kufurahia,” alisema Said.
Hata hivyo, baadhi ya watu waliohojiwa juu ya hatua hiyo inayotarajiwa kutekelezwa kesho, waliomba muda uongezwe huku walilaumu kitendo cha mamlaka zinazohusika kufumbia macho uingizaji wa simu bandia kuwa ni adhabu kwa watu wenye kipato cha chini.
Wateja wawa makini
Hata hivyo katika maeneo mbalimbali, mwandishi alishuhudia umakini kwa wanaonunua simu ambao wengi walikuwa wakilazimika kutumia kanuni iliyotolewa na TCRA, kubaini kama simu anayonunua ni bandia au halisi.
Wakiwa kwenye gulio la simu lililoandaliwa na kampuni za simu jijini Dar es Salaam hivi karibuni, walionekana watu wengi waliokuwa wakinunua simu za gharama nafuu huku wakihoji maswali kuhusu uhalali wake. Kampuni zatoa ofa Kampuni zinazotoa huduma za simu zimesema zinaendelea kusambaza simu za gharama nafuu nchini na kutoa ushauri kwa wateja .
Alipohojiwa juu ya athari watakazopata wateja wenye simu feki baada ya simu zao kuzimwa, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Rosallyn Mworia alisema laini za wateja hazitaathirika, bali simu bandia wanazotumika ndizo hazitafanya kazi.
Wakati huo huo kampuni ya simu ya Airtel imetangaza ofa kwa watu wanaohitaji simu halali, kuendana na matakwa ya serikali ya wananchi wake kutumia simu zinazokubalika kiafya na zenye ufanisi mkubwa.
Katika taarifa yake iliyotolewa jana, kampuni hiyo imesema Airtel Tanzania imeanzisha ofa ya kununua kifurushi chenye thamani ya Sh 22,000 kupata simu ya bure.
Mkuu wa kitengo cha Intaneti, Gaurav Dhingra alisema: “Tunatambua kwamba baadhi ya wateja wetu bado wanatumia simu ambazo hazina uhalisia, hivyo wako katika hatari ya kuzimiwa simu zao hapo itakapofika siku ya Alhamisi, Juni 16 (kesho).”
Wizi wa simu basi
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari na wafanyabiashara wa maduka ya simu mjini Kigoma jana, Kaimu Meneja wa Kanda ya Kati wa TCRA, Esuvatie Masinga alisema teknolojia hiyo itasaidia kudhibiti wizi wa simu za mkononi nchini.
Alisema simu itakayoibwa na kutolewa taarifa, itafungwa na haitaweza kutumika mahali popote duniani. Alisema teknolojia hiyo itadhibiti matumizi mbalimbali yasiyofaa ya simu za mkononi, ikiwemo wanaotukana, wanaotuma picha chafu na matumizi mengine yanayokatazwa.
Masinga alisema simu inapoibwa, utambulisho wa simu hiyo utaonekana kwenye laini nyingine itakayowekwa iwapo simu hiyo itaendelea kutumika. Mtu aliyekuwa na simu hiyo, atafuatiliwa na kukamatwa.
Sambamba na hilo, Meneja huyo alisema kuwa mfumo huo, unatoa faida kwa wanunuzi wa simu, ambao watapaswa kupewa garantii ya mwaka mmoja ya matumizi, jambo linalowalazimisha wafanyabiashara wanaouza simu kuuza simu halisi na siyo bandia.

Meneja huyo wa TCRA alisema simu zote na vifaa vyote vya mawasiliano ambavyo ni bandia, vitazimwa kama ambavyo imeshatangazwa awali na hakuna muda wa nyongeza kwa simu bandia kuendelea kutumika.
Akifungua mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Emanuel Maganga alisema udhibiti wa Mfumo wa Rajisi wa Simu za Mkononi, utasaidia kudhibiti uuzwaji wa simu holela, ambao unachangia kuwafanya wafanyabiashara kukwepa kukodi.

Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa alishauri bei za simu iwe ambayo wananchi wote watamudu. Aliomba mamlaka isimamie hilo, kuhakikisha linatekelezeka.

0 comments:

Post a Comment

TANGAZA HAPA KWA BEI NAFUU