test

Wednesday, May 9, 2018

Israel Yasema Itamuua Rais Assad wa Syria

Mmoja  wa mawaziri walio katika Kamati ya Usalama ya Baraza la Mawaziri Israel amesema wanaweza kuupindua utawala wa Rais, Bashar al Assad na kumuua iwapo Iran itatumia ardhi ya Syria kuishambulia Israel.

Waziri huyo wa Nishati, Yuval Steinitz amenukuliwa na mtandao wa habari wa Israel, Ynet akisema Israel haijajiingiza katika vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Syria hadi sasa.

Lakini alionya iwapo Rais Assad ataendelea kuiruhusu Iran kuendesha shughuli zake katika ardhi ya nchi hiyo Israel itammaliza na kuundoa madarakani utawala wake.

Kadhalika Waziri huyo ameendelea kueleza ikiwa Rais Assad atairuhusu Iran kuigeuza Syria kambi ya kijeshi dhidi ya Israel anapaswa kufahamu huo utakuwa mwisho wake.

Israel na Iran zimekuwa zikishambuliana katika vita maneno kuhusu Syria tangu Februari mwaka huu 

Aprili 9 mwaka huu shambulio la anga liliua askari sita wa kikosi cha makomando cha Revolutionary Guards cha Iran kambini nchini Syria.

Tehran iliilaumu Israel na kuapa kulipa kisasi, kauli iliyojibiwa na Israeli kuwa itafanya mashambuilizi makubwa dhidi ya miliki za Iran nchini Syria.

Pia Waziri Steinitz alionekana kugusia kuwa kauli yake haiakisi sera ya Serikali ya Israeli, akisema: ‘Sizungumzii kuwapo mkakati wowote kumhusu.”

Hakukuwa na mwitikio wa haraka kutoka ofisi ya Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu wala Wizara ya Ulinzi Israel kuhusu kauli hiyo nzito.

Iran, wanamgambo wa Lebanon, Hezbollah na Urusi zimekuwa zikiimarisha usaidizi wao kwa Damascus dhidi ya uasi wa miaka saba nchini Syria.

Lakini Israel inahofia uwapo wa maadui wake Iran na Hezbollah utatengeneza jeshi nchini humo litakalotishia usalama wake.

0 comments:

Post a Comment

TANGAZA HAPA KWA BEI NAFUU