test

Tuesday, May 8, 2018

Serikali Yawahamasiha Wananchi kuwekeza Katika Viwanda vya Kusindika Mazao

Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma
Serikali  imewataka wananchi kushiriki kikamilifu uanzishwaji wa viwanda vidogo vya kusindika vitunguu Saumu  na Mazao mengine ya Biashara katika maeneo yote hapa nchini.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Martha Umbulla, Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage amesema kuwa mazao ya Pareto na Vitunguu saumu yanayolimwa katika Wilaya ya Mbulu na maeneo mengine yana thamani kubwa na yanaweza kuchochea na kuhamasisha uanzishwaji wa viwanda vya kusindika mazao hayo.

“ Kwa kutambua faida zitokanazo na zao la pareto, Serikali iliamua kuanzisha Bodi ya Pareto kwa lengo la kudhibiti uzalishaji, usindikaji wa biashara ya pareto hapa nchini” Alisisitiza Mhe. Mwijage

Akifafanua amesema kuwa Serikali itaendeleza juhudi za kuhamasisha uwekezaji kwenye viwanda vya kuengua na kuchuja pareto ili kuongeza thamani ya zao hili na kuwanufaisha wananchi katika maeneo yanayolima pareto ikiwemo Wilaya ya Mbulu.

Kwa upande wa zao la Vitunguu saumu Wizara ya Viwanda kupitia karakana za SIDO katika mkoa wa Arusha na Kilimanjaro zinatengeneza  “Blender” ambayo itatumika kusaga zao hili kuwa katika mfumo laini ‘’ Garlic Paste” teknolojia hiyo inapatikana kwa gharama ya shilingi milioni moja na laki nane.

Aidha, SIDO imekuwa ikitoa mafunzo kwa vikundi na watu binafsi juu ya usindikaji wa zao la vitunguu saumu katika mikoa inayolima zao hilo.

Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli imekuwa ikihamasisha na imefanikiwa katika kuvutia wawekezaji na wananchi kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa viwanda hapa nchini.

0 comments:

Post a Comment

TANGAZA HAPA KWA BEI NAFUU